Soko la Kariakoo kuwa la Kimataifa zaidi

SERIKALI imeendelea kuwahakikishia wafanyabiashara wa Soko la Kariakoo kuwa la Kimataifa zaidi, kutokana na uboreshwaji inaoenda kufanyika katika soko hilo, kwa kuweka Miundombinu rafiki kwa watu wote wanaofika katika soko hilo kutoka pembe zote za Afrika Mashariki, kupata huduma masaa 24 na uimarishaaji wa ulinzi.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Machi 27, 2024 Ofisini kwake Jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Mhe. Edward Mpogolo, amesema wamekuwa na vikao mbalimbali na viongozi wa Wafanyabiashara pamoja na Machinga, lengo likiwa ni kufahamu changamoto mbalimbali zinazowakumba Wafanyabiashara hao katika soko la Kariakoo.


Wote tunajua ukubwa wa soko hili na mahitaji mbalimbali ambayo watu wamekuwa wakijipatia na kufanya idadi kubwa ya wateja kufika sokoni hapo, hivyo lazima na serikali kwa kushirikiana na Mwenyekiti wa Wafanyabiashara na Mwenyekiti wa Wamachinga kuhakikisha wanabainisha changamoto zao ili ziweze kupatiwa ufumbuzi wa haraka kabla ya kukarabatiwa kwa soko hilo.” amesema Mhem Mpogolo.

Aidha amesema, kikao hicho kimekuwa na makusanyo ya changamoto, ikiwemo wafanyabiashara kuegesha biashara zao nje ya maduka na kurasimisha kama eneo sahihi la kuendesha biashara hizo na kuleta ugumu kwa kupatikana njia katika soko hilo.

Unakuta Muuza magodoro ameweka bidhaa hizo dukani na pia ametoa hadi nje ya duka lake na kusababisha mrundikano wa bidhaa hizo hadi sehemu ya barabarani ,alikadhalika wauzaji wa Mafriji ni hivyo hivyo na inasababisha changamoto ya kulipa kodi sahihi na kupunguza thamani ya soko la Kariakoo” ameongeza.


Hata hivyo, Mhe. Mpogolo ameeleza kuwa, Serikali imeadhimia kuanza mara moja ukarabati wa soko hilo kwa kuanza kuweka taa na tayari baadhi ya mitaa imeshaanza kuweka taa hizo ikiwemo Mtaa wa Mkunguni na mchikichini na taa hizo zitawekwa mtaa wa Tandamti na Nyamwezi.

Kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi tunatekeleza hatua hizo za ukarabati wa awali wa kuweka taa hizo ili kuwepo kwa usalama zaidi kwa wateja ambao wanafika muda ambao wa jioni zaidi ama usiku hivyo itawarahisishia kuwepo kwa mwanga ambao kimsingi itawajengea amani na usalama eneo hilo kwa mteja au mfanyabiashara mwenyewe.” ameongeza.

Pia amesema, katika kikao hicho wamefikia muafaka wa kuhakikisha wafanyabiashara wa kushusha mizigo (Kirikuu) kupatiwa eneo stahiki la kushusha mizigo yao ili kuepusha misongamano pamoja na wafanyabiashara wanaoweka bidhaa zao chini watatakiwa kurudi kwenye maeneo yao rasmi waliyokwisha pangiwa.

Hata hivyo Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Jomaary satura, ameongeza kuwa jambo hilo la mkakati wa ukarabati wa soko hilo limekuwa shirikishi na limeweza kujadili changamoto mbalimbali kwakina na kwa pamoja tumeona tusipochukua hatua hizi kwa haraka na kwa ufanisi hatutaweza kufikia malengo ya soko la Kimataifa.


Pia amesema ukarabati huo utawawezesha wafanyabiashara hasa kipindi hiki cha kuelekea sikukuu kupata mahitaji masaa 24 kwa usalama zaidi kutokana na kuwepo kwa taa na kamera.

Kwa Upande wake Makamo Mwenyekiti wa Wafanyabiashara soko la Kariakoo, Steven Lusinde, ametoa pongeza kwa Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ndani ya Miaka mitatu imekuwa ya Maendeleo na mabadiliko katika sekta mbalimbali na kuwaona wafanyabiashara wanahitaji maboresho mbalimbali, ili waweze kufanya biashara zao kwa ufanisi zaidi .

Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi