Mkuu wa Mkoa wa DSM awataka Wakandarasi kufanya Kazi kwa Uadilifu

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Albert Chalamila amewataka wakandarasi wanaopewa kazi za ujenzi wawe waadilifu na wazifanye kazi hizo kwa uweledi mkubwa kama walivyoaminiwa na Serikali na ikitokea mkandasi anaona hana mtaji wa kutekeleza mradi ni vizuri asichukue tenda hiyo. Wito huo ameutoa leo Mei 29, 2024 Jijini Dar es Salaam wakati akiendelea na ziara ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Jiji la Dar es Salaam katika Jimbo la Ilala.


Akizungumza wakati wa ukaguzi wa ujenzi wa Kituo cha Afya Mchikichini Mhe. Chalamila amesema “Kipekee namshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa pesa kiasi cha Billioni 5.2 kwaajili ya kituo hiki cha afya, lakini pia niwashukuru Mkuu wa Wiaya na Mkurugenzi wa Jiji kwa kusimamia Mradi huu ambao utaenda kusaidia wananchi wa Kata za jirani kupata huduma za afya kwa wakati ,hivyo nimtake mkandarasi kutoka Sky Construction wakishirikiana na Humphrey Construction kukamilisha jengo hili kwa wakati ili wananchi wetu waweze kupatiwa huduma za afya kwa wakati na kwa ukaribu zaidi pamoja na kuhakikisha malengo ya Serikali ya kuanzisha mradi huu wa kusogeza huduma muhimu karibu na jamii yanatimia."


Aidha, amemuagiza Mkuu wa Wilaya kuunda kamati maalumu itakayochunguza mwenendo wa utendaji kazi katika Kituo hicho cha afya ili kubaini changamoto zilizopo na kutoa mapendekezo ya Mambo ya kufanya ili kuboresha ujenzi huo.


Naye Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe. Edward Mpogolo ametoa shukrani zake kwa Mkuu wa Mkoa kwa ziara anazoendelea kufanya za kukagua Miradi ya Maendeleo pamoja na kuongea na wananchi huku akimuhakikishia kutekeleza yote aliyoyaagiza.


Kituo hicho cha ghorofa tano kinajengwa kwa kiasi Cha shilingi Bilioni 5.2, ikiwa ni Fedha kutoka Mapato ya Ndani ya Halmashauri na Fedha kutoka Serikali Kuu na pindi kikikamilika kinatarajiwa kuwa msaada mkubwa kwa wananchi wasiopungua elfu nane wa Kata za Wilaya ya Ilala pamoja na wananchi kutoka Wilaya za Jirani za Mkoa wa Dar es Salaam.


Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi