Wakazi wa Gongolamboto wahimizwa kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura

Mstahiki Meya wa jiji la Dar es salaam Mhe. Omary Kumbilamoto amewasisitiza wakazi, wazazi, walezi pamoja na wanafunzi wenye sifa ya kupiga kura kujitokeza kwa wingi kujiandikisha kwenye daftari la mpiga kura la Uchaguzi wa Serikali za Mitaa Ili waweze kushiriki uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024 kwa kuchagua viongozi wanaowapenda.


Mhe. Kumbilamoto ameyasema hayo leo octoba 10, 2024 wakati akizungumza na Wananchi waliojitokeza katika sherehe ya mahafali ya 20 ya kidato cha nne ya shule ya Sekondari Juhudi yaliyofanyika katika viwanja vya shule hiyo Jijini Dar es salaam.


Nipende kutumia nafasi hii kuwakumbusha wananchi wote mliojitokeza katika sherehe hii ya mahafali, wenye sifa za kupiga kura mjitokeze kwa wingi katika Zoezi la kujiandikisha kwenye Daftari la mpiga kura la Uchaguzi wa Serikali za Mitaa katika maeneo yenu , Zoezi hili linatarajia kuanza siku ya kesho tarehe 11 hadi 20 octoba 2024 ambalo litadumu kwa muda wa siku kumi” amesema Mhe. Kumbilamoto.


Sambamba na hilo, Mhe. Kumbilamoto amewataka wazazi na walezi wa wanafunzi hao kusimamia malezi bora na usalama wa watoto hao wanapokua nyumbani ili kujenga kizazi chenye maadili huku akiwahakikishia viongozi wa Shule kutatua changamoto ya upungufu wa madarasa pamoja na uzio.


Awali akisoma Risala, Mkuu wa shule ya Sekondari Juhudi Mwl.  Happiness Pallangyo ameeleza kuwa Shule ya Sekondari Juhudi imekua ikifanya vizuri katika eneo la taaluma na nidhamu kwa ujumla kwani wanafunzi wa Shule hiyo wamekuwa wakifanya vizuri toka 2022 hadi sasa huku akisisitiza kuendelea kusimamia maadili na nidhamu kwa watoto Ili kuendelea kuongeza ufaulu.


Sambamba na hilo, Mwl. Pallangyo ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa fedha anazoendelea kuzitoa katika kuhakikisha sekta ya Elimu inaendelea kukua huku akimshukuru Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam kwa kuendelea kuboresha miundombinu ya Elimu katika Shule ya Sekondari Juhudi na Shule zote za Jiji la Dar es Salaam.


Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi