Kamati ya Kudhibiti UKIMWI yafanya ziara ya kukagua Miradi ya Maendeleo

Kamati ya Kudhibiti UKIMWI ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam leo tarehe 15 Februari, 2023 imefanya ziara ya kukagua miradi ya maendeleo iliyotekelezwa ndani kwenye robo ya pili ya mwaka wa Fedha 2022/2023 (Oktoba mpaka Desemba 2022) ambapo Kamati hiyo imetembelea Zahanati ya Majohe iliyopo Kata ya Majohe ili kufahamu huduma zinazotelewa pamoja na ukaguzi wa ujenzi wa majengo mapya.


Akiongea kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Diwani wa Kata ya Liwiti Mjumbe wa Kamati ya Kudhibiti UKIMWI Mhe. Alice Mwangomo alitoa shukrani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa Fedha ambazo zimetolewa kukamilisha ujenzi wa majengo kwenye zahanati hiyo kwani itasaidia kuboresha huduma zitakazotolewa hapo.


"Tunaishukuru sana Serikali ya Awamu ya sita kwa kuweza kuipandisha hadhi zahanati hii na kuwa kituo cha Afya ambapo itaongeza wigo wa kuwafikia wananchi wengi zaidi wa Kata ya Majohe na maeneo ya karibu” aliongeza Mhe. Mwangomo

Nae, Mganga Mfawidhi wa Zahanati ya Majohe Dkt. Rosemary Amlima amesema kuwa ujenzi wa majengo mapya ambayo ni chumba cha upasuaji, wodi ya wazazi pamoja na maabara yamekamilika kwa asilimia 100 na wanatarajia mpaka kufikia mwisho wa mwezi huu wa pili yataanza kutumika rasmi huku jengo la OPD likiwa kwenye hatua za ukamilishaji.

Zahanati ya Majohe inatarajiwa kupandishwa hadhi na kuwa Kituo cha Afya pindi majengo yanayoendelea kujengwa kukamilika baada ya kupokea Sh. Milioni 500 fedha zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan maarufu kama ‘Pochi la Mama’



Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi