Jiji la DSM wapatiwa mafunzo ya utekelezaji wa Mradi wa Kijana Nahodha

Waheshimiwa Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam pamoja na Wataalamu wa Sekta ya Elimu na Maafisa Maendeleo ya Jamii, leo tarehe 02 Machi, 2023 wameshiriki katika kikao kazi cha uhamasishaji jamii kwa ajili ya mafunzo kupitia mradi wa Kijana Nahodha, unaotekelezwa kwa Halmashauri Tatu (3) kwa Mkoa wa Dar es Salaam.


Akiongea katika kikao hicho Meneja Mradi Kijana Nahodha kutoka T-MARC Ndugu Upendo Laizer ameeleza kuwa Mradi wa kijana Nahodha ni mradi uliozinduliwa na Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Dtk. Hussein Mwinyi, utadumu kwa kipindi cha miaka Mitano (5) kuanzia Septemba, 2022 hadi Agosti 2026.


Mradi huu unatekezwa na Shirika la T-MARC wakishirikiana na CARE Tanzania, Tanzania Youth Coalition (TYC), Y-LABS chini ya Shirika la Kimataifa kutoka Marekani (US AID) ambao umelenga kuwasaidia vijana kuanzia miaka 15 hadi 25 kutoka Zanzibar na Tanzania ambao walikatisha ndoto zao za masomo kwa matatizo mbalimbali.


Ameeleza Ndugu Upendo Laizer Sambamba na Hilo Mradi wa Kijana Nahodha umelenga kutekelezwa katika Mikoa miwili ambayo ni Morogoro na Dar es Salaam ambapo kwa Dar es Salaam Mradi huu utatekelezwa katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Halmashauri ya Manispaa ya Temeke pamoja na Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kwani katika utafiti maeneo haya yameoneka kuwa na vijana wengi zaidi ambao wanaishi katika mazingira magumu na hatarishi.


Naye Meneja Mradi Kijana Nahodha kutoka Care International Ndugu Samwel Chambi ameeleza kuwa “Mradi umeandaa vikao kazi kwa lengo la kuzindua rasmi uhamasishaji jamii ili kuwatambua na kuwaandikisha vijana katika vituo vya mafunzo ya serikali ya muda mfupi yaani Open School au QT katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kwa vijana wenye mahitaji maalumu, mazingira magumu, yatima, pamoja na wale wanaoishi na Virusi vya UKIMWI watapatiwa ufadhili ili kuweza kutimiza adhma yao ya kupatiwa elimu na ujuzi hivyo tunategemea mchango wenu kwa kuwahamasisha wanajamii waweze kuwaandikisha vijana hao katika ofisi za Serikali za Mitaa ili waweze kupata ufadhili huo wa masomo na ujuzi kwa lengo la kupata elimu na kuendeleza ndoto zao.


Sambamba na hilo Ndugu Chambi ameeleza kuwa kutakua na zoezi la uhamasishaji ambalo litafanyika tarehe 08 na 09 Machi 2023 katika Kata zote za Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kwa lengo la kuhamasisha zoezi hilo na kuweza kupata vijana hao.


Akiahirisha kikao hicho Mwenyekiti wa Kikao Mhe. Robert Manangwa ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Uchumi na Huduma za Jamii Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, amesema Nipende kutoa Shukrani zangu za dhati kwa waandaaji wa mradi huu kwa kuweza kuichagua Halmashauri yetu kati ya Halmashauri tatu zilizopendekezwa Nimatumaini yangu tutaenda kuutangaza huu mradi kwa wananchi wetu na tunawaahidi ushirikiano katika kutekeleza vyema mradi huu wa Kijana Nahodha.



Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi