Zoezi la upandaji Miti laendelea kwa Kasi Wilaya ya Ilala

Katika kuelekea siku ya upandaji miti Kitaifa ambayo hufanyika kila tarehe 1 Aprili Wilaya ya Ilala leo tarehe 31, Machi 2023 wameadhimisha siku ya upandaji miti kwa ngazi ya Wilaya ambapo miti 300 imeweza kupandwa katika Shule ya Msingi Muungano iliyopo Kata ya Kiwalani Jiji la Dar es Saalam.


Akiongoza zoezi hilo la upandaji miti kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Ilala Katibu Tawala wa Wilaya ya Ilala Bi. Charangwa Selemani amesema “Kutokana na mabadiliko ya tabia ya Nchi inatupasa tupande miti kwa wingi ili kukabiliana na changamoto hii hivyo sisi kama Wilaya ya Ilala tumeweza kupanda miti elfu 11 na leo hii katika maadhimisho haya ya siku ya upandaji miti ngazi ya Wilaya tumeweza kupanda miti 300 katika Shule ya Msingi Muungano huku miti hiyo ikiwa ni miti ya matunda kama Miembe, Michungwa, Mipera, Mikungumanga pamoja na miti ya Kivuli hivyo nitoe wito kwa Waalimu na Wanafunzi kuhakikisha miti hii inatunzwa vizuri ili iweze kukua kwa wakati na tutakuja kukagua kuona kama mnatekeleza haya”.


Sambamba na hilo Bi.Charangwa ametoa wito kwa Wananchi wote kuhakikisha wanapanda miti kwa wingi katika maeneo yao ya makazi lengo likiwa ni kutunza mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabia ya nchi. “ Kulingana na kauli mbiu ya siku ya upandaji miti kitaifa isemayo ‘Miti ni Afya’ pamoja na kutekeleza maagizo ya Makamu wa Raisi wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ya kila Wilaya kuhakikisha wanapanda miti Milioni 1.5 kila Mwaka natoa wito kwa wananchi wote wa Wilaya ya Ilala kuhakikisha mnapanda miti kwenye makazi yenu ili tuweze kufikia lengo letu hivyo sisi kama Wilaya tutaendelea kushirikia na Wadau mbalimbali kuhakikisha tunapanda miti kwa Wingi hasa maeneo ya hifadhi ya mito pamoja na maeneo ya pembezoni mwa barabara”.


Akiongea kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Afisa Elimu Msingi Bi.Siporah Tenga ameeleza kuwa katika kutekeleza kampeni ya soma na Mti wanafunzi kila mwanzafunzi atatakiwa kupanda mti wake na kuhakikisha anautunza vyema, “Sisi kama viongozi tutahakikisha tunasimamia vyema zoezi hilo na kwa ukaribu zaidi kuhakikisha miti hii inayopandwa inatuzwa vyema na kuangaliwa kwa ukaribu zaidi ili iweze kukua kama ilivyotarajiwa.”

Naye Mkuu wa Kitengo cha Maliasili na Uhifadhi wa mazingira wa Halmasahuri ya Jiji la Dar es Salaam Bi. Theresia Denis ameeleza kuwa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam imeendelea kutekeleza maelekezo ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 ya kuendeleza programu mbalimbali za upandaji miti na ufugaji nyuki ili kutunza mazingira na kuongeza kipato kwa wananchi na Taifa.


Sambamba na hilo Bi.Theresia ameendelea kusema “Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam imeweza kushirikiana na Wananchi pamoja na wadau mbalimbali kubaini aina ya miti itakayopandwa na maeneo gani miti hiyo ipandwe ambapo katika kutekeleza hilo miti hiyo itaweza kupandwa maeneo ya hifadhi ya mto Msimbambazi, Msitu wa zingiziwa, maeneo ya Shule, zahanati pamoja na vituo vya afya pia zoezi hili linaenda sambamba na uhamasishaji wa wanafunzi kushiriki katika zoezi la upandaji miti ili kuwajengea tabia ya kutunza na kuhifadhi mazingira”.


Kwa upande wake Afisa Elimu wa Kata ya Kiwalani Bi. Christina Abraham Machenje ametoa shukurani zake za dhati kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kupitia Idara ya Maliasili na auhifadhi wa Mazingira kwa kutuletea miti katika Shule ya Msingi Muungano kwani tunaahidi miti hii tutaitunza na itakua vyema hivyo nitoe wito kwa wananchi wenye mifugo ambayo huzurura maeneo ya Shule na kuharibu mazingira wahakikishe mifugo hiyo wanaifungia ndani lengo kuu ni kuhakikisha tunatunza mazingira ya Shule yetu kwa afya za watoto wetu.

Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi