Waziri Silaa afungua rasmi Ardhi Clinic ndani ya Wilaya ya Ilala

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Jerry Silaa amewapongeza Maafisa wa Ardhi kwa kupunguza migogoro ya Ardhi nchini. Hayo yamesemwa Leo Desemba 18, 2023 wakati wa uzinduzi wa Ardhi Clinic zoezi ambalo lipo chini ya Mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi (LTIP) unaofadhiliwa na Benki ya Dunia na kusimamiwa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi katika Kata ya Chanika, zoezi litakalodumu kwa muda wa siku 25.


Mhe. Silaa amesema “Nawapongeza maafisa wa Ardhi kwa kazi nzuri mliyoifanya tangu mlipopewa siku 100 za kupunguza migogoro ya Ardhi , mmefanya kazi usiku na mchana kuhakikisha maelekezo yaliyotolewa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan yanatekelezwa na kero za wananchi zinatatuliwa."


Aidha, amesema lengo la kuanzisha Clinic ya Ardhi ni kuwapunguzia wananchi muda na umbali wa kushughulikia masuala ya Ardhi ikiwemo kutatua changamoto zote zinazokabili urasimishaji ardhi ikiwemo kupanga na kupima maeneo yanayoyohitaji leseni za makazi na hati Miliki, kurahisisha gharama za upimaji, kutoa hati na leseni za makazi pamoja na kuboresha miundombinu ya ardhi kwa nchi nzima.


Akitoa takwimu ya mwenendo wa zoezi hilo, Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Dar es Salaam Ndg. Shukrani Kyando amesema kuwa wamekwishafanya zoezi hilo katika Wilaya za Temeke, Kigamboni, Ubungo na Sasa wameingia Ilala ambapo zoezi hilo limefanikiwa kwa kiasi kikubwa kwani mwitikio wa wananchi ni mkubwa na mpaka Sasa hati za viwanja 5784 zimekwishatolewa kwa wananchi, migogoro ya Ardhi ipatayo 7462 imekwishapatiwa ufumbuzi na kiasi Cha Shilingi Milioni 753 kimekusanywa tangu kuanzishwa kwa zoezi hili ndani ya mkoa wa Dar es Salaam.



Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi