Walimu Shule ya Sekondari Juhudi wapongezwa

Diwani wa Kata ya Gongolamboto Mhe. Lucas Rutainurwa amewapongeza walimu wa Shule ya Sekondari Juhudi kwa juhudi wanazozifanya ikiwa ni pamoja na kuongeza ufaulu wa wanafunzi wa kidato cha nne kwa mwaka 2023.


Pongezi hizo zimetolewa leo Februari mosi, 2024 wakati wa halfa fupi ya kuwapongeza walimu iliyoambatana na utoaji wa zawadi, iliyofanyika katika shule hiyo iliyopo Wilaya ya Ilala Jijini DSM.

Akiongea na wanafunzi, walimu pamoja na wazazi/walezi Mhe. Rutainurwa amesema "Napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa uongozi wa shule. Pia nawapongeza walimu kwa jitihada zao kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu iliyokusudiwa, ufaulu umeongezeka kwa kiasi kikubwa ukilinganisha na miaka iliyopita, hivyo walimu wanasikiliza na kutekeleza ushauri na maoni kutoka kwa viongozi na wazazi, ni kazi ngumu lakini hawakati tamaa, wazazi pia tusiache kufatilia maendeleo ya watoto wetu shuleni. Bado kuna kazi kubwa ya kufanya kuhakikisha wanafunzi wote wanafaulu na kuendelea na masomo ya juu hivyo niwaase kuendeleza jitihada hizi."


Awali akifungua halfa hiyo Mkuu wa Shule hiyo Mwl. Happiness Pallangyo amemshukuru Mhe. Rutainurwa kwa kushiriki katika halfa hiyo, pia amesema halfa hii iwe chachu kwa wanafunzi wengine kufanya vizuri katika masomo na mitihani yao.


"Hafla hii ni kwaajili ya kutambua juhudi na jitihada kubwa walizofanya walimu wetu kwenye mitihani ya kidato Cha nne mwaka 2023. Tunaamini tukio hili litaleta hamasa na chachu ya watu kujituma ili mwaka huu tuweze kufanya vizuri zaidi.

Lakini pia niwatake walimu mliopata zawadi kutobweteka badala yake muendelee kujituma Zaidi kwa maendeleo ya shule yetu." Ameongeza Mwl. Pallangyo.


Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi