Na: Hashim Jumbe
Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe. Sophia Mjema, leo tarehe 28 Aprili, 2017 amefanya uzinduzi wa Bodi na Kamati mpya zitakazoshiriki katika uendeshaji na usimamizi wa utoaji huduma za afya katika vituo vya afya vinavyosimamiwa na Halmashauri ya Manispaa ya Ilala.
Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe. Sophia Mjema, leo tarehe 28 Aprili, 2017 amefanya uzinduzi wa Bodi na Kamati mpya zitakazoshiriki katika uendeshaji na usimamizi wa utoaji huduma za afya katika vituo vya afya vinavyosimamiwa na Halmashauri ya Manispaa ya Ilala.
Uzinduzi huo wa Bodi na Kamati za huduma za afya ni matokeo
ya mabadiliko katika mfumo wa uendeshaji wa huduma za afya yaliyoanza mwaka
1993/1994 yanayolenga kuhamasisha Jamii kumiliki huduma za afya na kuiwezesha
Jamii kupanga, kuendesha, kusimamia na kutathmini utoaji wa huduma za afya
katika Jamii.
Akiongea na Wajumbe wa Bodi na Kamati za huduma za afya wakati
wa uzinduzi huo, Mhe. Mjema alisema “kuundwa kwa Bodi na Kamati za huduma za
afya katika vituo vya tiba ni fursa muhimu katika kuendelea kuboresha na
kuimarisha utekelezaji wa mkakati wa huduma za afya ya msingi katika Wilaya
yetu kwa kushirikisha Jamii”.
Naye, Mganga Mkuu wa Manispaa ya Ilala, Bi. Victorina
Ludovick awali aliwasilisha taarifa inayoonesha mafanikio ya uanzishwaji wa Bodi na Kamati za
huduma za afya kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2010-2016, ambapo Mganga Mkuu
alisema “uanzishwaji wa Bodi na Kamati za huduma za afya umefanikisha mambo
kadhaa, ikiwa ni pamoja na kufanikisha suala la kupunguza vifo vya Mama
wajawazito kutoka vifo 37 mwaka 2010 hadi vifo 19 mwaka 2016, vifo vya Watoto
wachanga navyo vimepungua kutoka 309 kwa mwaka 2012 hadi vifo 205 mwaka 2016”.
Aidha, Bi. Victorina aliendelea kueleza mafanikio mengine
yaliyopatikana kutokana na kuanzishwa kwa Bodi na Kamati za afya kuwa ni
kuongezeka kwa fedha za uchangiaji kutoka Tsh. 50,000/= kwa mwezi mwaka 2006
hadi Tsh. 600,000/= kwa mwezi mwaka 2016 katika vituo vidogo na Tsh. 2,900,000/= hadi Tsh. 15,000,000/= kwa vituo
vikubwa.