MKURUGENZI MANISPAA YA ILALA AWAASA WANAFUNZI 120 WALIOINGIA KAMBINI KUJIANDAA NA UMITASHUMTA

Na: Hashim Jumbe


Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, ambaye pia ni Mwenyekiti wa UMITASHUMTA Wilaya ya Ilala, Ndugu Msongela Palela, amewaasa Wanafunzi 120 walioingia kambini kujiandaa na mashindano ya UMITASHUMTA kuzingatia nidhamu na maelekezo mengine watakayopewa na Wasimamizi wao.

Nasaha hizo za Mkurugenzi amezitoa wakati akiwaaga Wanamichezo hao kabla ya kuingia kambini kujiandaa na mashindano yanayotarajiwa kuanza siku ya Jumanne ijayo kwa Kanda ya Dar-es-Salaam.

“Nidhamu ndiyo kila kitu kwenu, nataka safari hii kikombe cha ushindi wa nidhamu kije kwetu Wilaya ya Ilala, mkazingatie maagizo ya Walimu wenu, mcheze kwa bidii na mtakaporudi nitakuja kuwapokea, na ninawaahidi kuwapa zawadi ya kwangu Mkurugenzi” alisema Mkurugenzi Palela.

Aidha, Mkurugenzi Palela aliendelea kuwasisitiza Wanafunzi hao pamoja na kujituma kwenye michezo wakumbuke pia kufanya jitihada kwenye taaluma “Mimi leo ni Mkurugenzi wenu, najisikia faraja sana Ofisini kwangu wanapokuja Walimu walionifundisha na kuwasaidia, natamani na nyie siku moja muwe Wakurugenzi na mje mnisaidie, muwasaidie na Walimu wenu”

Wakati huo huo, Afisa Elimu Msingi Manispaa ya Ilala, Bi.Elizabeth Thomas ametoa motisha kwa Wachezaji hao kwa kununua kila goli litakalofungwa kama alivyofanya mwaka jana “mwaka jana mlishinda makombe saba, nataka na mwaka huu mkashinde makombe yote, na ninatoa ahadi ya kununua kila goli, mwaka jana kikombe cha nidhamu kilienda Kinondoni, sasa nataka mwaka huu kije Ilala”.

Ikumbukwe, mashindano ya umoja wa michezo na taaluma kwa shule za msingi Tanzania (UMITASHUMTA) yalianza kwa ngazi Kata, Klasta, Wilaya na sasa ni ngazi ya Mkoa na ngazi ya Kitaifa mashindano yanatarajiwa kufanyika Jijini Mwanza katikati ya mwezi Juni.  













Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi