UFAHAMU MRADI WA UENDELEZAJI WA JIJI LA DSM ‘DMDP’ UTEKELEZAJI WAKE NA MAFANIKIO KWA WANANCHI WA MANISPAA YA ILALA


Na: Hashim Jumbe
KWA mujibu wa Sensa ya Watu na makazi ya mwaka 2012, Dar es Salaam inakadiriwa kuwa na Watu wapatao Milioni 4.3, huku idadi hiyo ikitazamiwa kuongezeka hadi kufikia Watu Milioni 10 ifikapo mwaka 2030, hivyo kulifanya Jiji la Dar es Salaam kuwa kati ya Majiji yanayoongoza kwa ukubwa na makazi mengi.

Sambamba na ongezeko hilo, lakini pia Jiji la Dar es Salaam ndiyo Jiji linalochangia kwa asilimia kubwa katika ukuaji wa pato la Taifa na kuwa lango la biashara kwa Mataifa ya jirani, huku Jiji hilo likikabiliwa na changamaoto ya ubora wa Miundombinu, hivyo kuzorotesha baadhi ya shughuli na kuwa kikwazo kwa ustawi wa Jiji na Taifa kwa ujumla.

Aidha, kasi ya ukuaji wa Jiji la Dar es Salaam haiendani na Miundombinu iliyopo kwani inakadiriwa kuwa asilimia kati ya 70 hadi 80 ya makazi ya Jiji la Dar es Salaam hayajapimwa, hivyo kutokana na ukuaji huo na mabadiliko ya tabia nchi yanayoikabili Dunia, athari za mafuriko zinatarajiwa kuongezeka katika Jiji la Dar es Salaam, kwa hali hiyo bila ya kuwa na mipango bora ya utoaji wa huduma, Jiji hili linaweza kutokukalika.

Ili kukabiliana na changamoto hizo, Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ndipo ilipokuja na wazo la kuwa na Mradi wa Uendelezaji wa Jiji la Dar es Salaam ujulikanao kama ‘Dar es Salaam Metropolitan Development Project’ ama unaweza kuuita kwa kifupi DMDP.

Aidha, Mradi wa DMDP ni matokeo ya miradi miwili mikubwa inayotekelezwa na Serikali ya Tanzania. Mradi wa kwanza ni ule wa uendelezaji wa Miji minane kimkakati (Tanzania Strategic Cities Project – TSCP) unaotekelezwa katika Majiji ya Arusha, Mwanza , Tanga na Mbeya na Manispaa za Kigoma Ujiji, Mtwara Mikindani, Dodoma pamoja na Mamlaka ya Uendelezaji wa Makao Makuu Dodoma – CDA.

Mradi mwingine ni ule wa Uendelezaji Miji kumi na nane ujulikanao kama Urban Local Government Strengthening Programme (ULGSP). Kwa ujumla miradi hii yote mitatu ina lengo la kuboresha miundombinu ya barabara, mitaro ya maji ya mvua, nyenzo muhimu za ukusanyaji na uhifadhi wa taka ngumu pamoja na mifumo ya ukusanyaji wa mapato ya ndani katika maeneo husika vimeboreshwa kwa kiwango kikubwa.
Maandalizi ya mradi wa DMDP
Maandalizi ya Mradi wa DMDP ambao umeanza kutekelezwa katika Manispaa zote za Jiji la Dar es Salaam yalianza katika kipindi cha mwaka wa Fedha 2012/2013 kwa Manispaa za Jiji la Dar es Salaam kuibua vipaumbele kuanzia ngazi ya chini na kufuatiwa pembuzi na sanifu zilizofanywa na Washauri waelekezi mbalimbali.
 Vigezo muhimu vilivyozingatiwa vilikuwa ni hivi vifuatavyo:-
i)  Miradi inayounganisha maeneo ya Watu wenye kipato kidogo na yaliyojengwa holela
ii) Miradi inayounganisha Wilaya na Mkoa
iii) Miradi inayounganisha maeneo mbalimbali na ukanda wa mabasi yaendayo haraka (BRT) ili kurahisisha usafirishaji

Kwa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, vigezo hivyo vitatu viliibua miradi ifuatayo;
i)  Ujenzi wa barabara za mlisho (feeder roads) zenye urefu wa kilometa 3.2
ii) Ujenzi wa mifereji ya kutiririsha maji ya mvua yenye urefu wa kilometa 15.96 katika mabonde ya mto Msimbazi na Yombo
iii) Kupandisha hadhi makazi yaliyopangwa kiholela katika Kata za Gongolamboto, Kiwalani, na Ukonga, kuweka nyenzo za ukusanyaji wa taka ngumu, kujenga mitaro ya kutiririsha maji ya mvua, kuweka taa za barabarani, kujenga njia za watembea kwa miguu, ujenzi wa maeneo ya mapumziko na vituo vya mabasi, ujenzi wa vyoo vya umma na ujenzi wa maeneo ya michezo.
iv) Kuandaa Mpango kabambe wa Mfumo wa Maji ya Mvua na Maji Taka (Storm Drainage and Sewerage Master plan)
v) Kundaa Mpango Mkakati wa kuendeleza Ukanda wa mabasi yaendayo haraka (BRT Corridor Development Strategy). Kwa kushirikisha Sekta Binafsi;  kujenga masoko ya kisasa na ya kawaida, kujenga maduka makubwa (shopping malls) na ya kawaida, kuboresha maeneo ya utalii, kujenga maeneo maalum ya maegesho, kuweka njia za waendesha baiskeli na watembea kwa miguu n.k
vi) Kufunga mfumo wa kisasa wa ukusanyaji wa mapato wa Halmashauri
vii) Kujenga uwezo wa mwitikio wa haraka katika kukabiliana na majanga.

Utekelezaji wa Mradi wa DMDP kwa Manispaa ya Ilala
Kwa ujumla utekelezaji wa Mradi wa DMDP umepangwa kufanyika katika awamu mbili. Awamu ya kwanza imeanza kutekelezwa katika kipindi cha miaka mitano kuanzia 2016 mpaka 2020 na awamu ya pili inatarajiwa kutekelezwa kuanzia mwaka 2020 mpaka 2025 kadri ya makubaliano kati ya Serikali ya Tanzania na Benki ya Dunia.
Manispaa ya Ilala imetengewa Shilingi Bilioni 115 kwa mradi wote na hadi sasa imeingia mikataba yenye thamani ya Shilingi Bilioni 49.84 katika kujenga Kilometa 25.84 za barabara za lami, kujenga masoko 3, kujenga maeneo ya mapumziko, kujenga mifereji ya chini ya Kilometa 2.8 (underground storm drainage), kuweka huduma za vyoo vya Umma na maji safi.
Aidha, Shilingi Bilioni 65.16 zimepangwa kujenga barabara ya Ulongoni Bangulo-Kinyerezi yenye urefu wa Kilometa 7.5 na kujenga mifereji mikubwa ya maji yenye urefu wa Kilometa 15.96 pamoja na bwawa la kukinga maji kwa muda (Detention pond)
 
Jengo la ghorofa moja la Ofisi ya DMDP Manispaa ya Ilala lililopo Arnatoglou-Mnazi Mmoja
Hadi kufikia Machi, 2018 kwa Manispaa ya Ilala mradi wa DMDP umetekelezwa kama ifuatavyo;
i.      Ujenzi wa barabara za Mlisho (feeder roads) zenye urefu wa Kilometa 3.2 ambazo ni Ndanda yenye urefu wa Kilometa 0.35, Kiungani Kilometa 0.68, Omari Londo Kilometa 0.53, Olympio Kilometa 0.68, Mbarouk Kilometa 0.38 na barabara za Kongo, Livingstone, Swahili na Nyamwezi zenye jumla ya urefu wa Kilometa 0.58. Pamoja na barabara hizo, lakini pia ujenzi wa mifereji ya chini (underground storm drainage) yenye urefu wa Kilometa 0.58 imekamilika sambamba na ujenzi wa Ofisi na maabara ya kisasa. Gharama zilizotumika hadi sasa ni Shilingi Bilioni 7.18
Moja kati ya barabara za mlisho iliyojengwa Kata ya Upanga Mashariki, barabara ya Olympio inavyoonekana kwa sasa baada ya kujengwa kupitia Mradi wa Uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam 'DMDP'


ii.   Ujenzi wa barabara kwenye makazi yasiyopangwa Kata ya Gongolamboto ambapo ujenzi huo ulianza tangu tarehe 1 Novemba, 2017 ambapo ujenzi umeanza kwenye barabara za Chung'e iliyo na urefu wa Kilometa 1.49, barabara ya Kampala Kilometa 2.06, Limbanga 2.44, High Mount Kilometa 1.44 na Baghdad Kilometa 0.34. Aidha Kata ya Gongolamboto pia unajengwa mtaro wenye urefu wa Kilometa 1.85, vizimba 7 vya taka na kununua garimoja la kusomba taka. Gharama zilizotumika hadi sasa ni Bilioni 3.05
Barabara ya Kampala yenye urefu wa Kilometa 2.06 nimoja kati ya barabara zilizojengwa kwenye maeneo yasiyopangawa kwenye Kata ya Gongolamboto

iii. Ujenzi mwengine ni kwenye barabara zilizopo kwenye makazi yasiyopangwa Kata ya Kiwalani ambapo barabara zenye urefu wa Kilometa 10.35 zinaendelea kujengwa, barabara hizo ni zile za Bush iliyo na urefu wa Kilometa 1.07, Gude Kilometa 1.33, Jongo Kilometa 0.4, Mbilinyi Kilometa 0.35, Pepsi Kilometa 0.59, Jamaka Kilometa 0.62, Zahanati Kilometa 1.17, Kamungu Kilometa 1.21, Mkwajuni Kilometa 1.16, Binti Musa Kilometa 2.14 na Betheli Kilometa 0.31
Barabara ya Gude yenye urefu wa Kilometa 1.33 ni moja ya kati ya barabara zilizojengwa kwenye Kata ya Kiwalani

iv.   Aidha, Kata ya Kiwalani pia itanufaika na ujenzi wa vituo vitatu vya kutolea huduma za vyoo, vizimba 8, kununua gari 1 la kusombea taka,kujenga masoko matatu, kujenga maeneo ya kupumzikia mawili na kujenga vituo vitatu vyaa kutoleaa huduma za maji safi. Hivyo jumla ya fedha zilizotumia kwa Kata hii ya Kiwalani hadi sasa Shilingi Bilioni 2.8
v.    Kata nyengine inayonufaika na Mradi huu wa DMDP ni Ukonga ambapo hadi sasa maeneo yaliyotekelezwa ni ujenzi wa barabara ya Kilometa 12.29 kwenye makazi yasiyopangwa ambapo zinajengwa barabara za Markaz yenye urefu wa Kilometa 1.86, Zimbili yenye urefu wa Kilomita 3.02, Dispensary yenye urefu wa Kilometa 1.06, School yenye urefu wa Kilometa 2.18 na Chacha Kilometa 3.17
Ujenzi wa baraba ya Zimbili iliyo na urefu wa Kilometa 3.02 ukiendelea 

vi.   Ujenzi mwengine kwa Kata ya Ukonga ni wa vituo 7 kwa ajili ya Wananchi kupata huduma safi za maji na ujenzi wa vizimba 9 vya taka, hivyo kufanya jumla ya gharama iliyotumia kwa Kata hiyo hadi sasa kufikia Shilingi Bilioni 2.95


Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi