UONGOZI NA DIRA YA MAENDELEO

 Na Mwandishi wetu

Uongozi ni mamlaka au karama anayopewa mtu kuwaonyesha watu njia kwa vitendo. Kipimo cha uongozi ni namna ambavyo kiongozi anaweza kuleta ushawishi kwa watu na kufikia maendeleo yaliyotarajiwa.

Katika matoleo ya jarida hili tutakuwa na mfululizo wa makala kuhusu uongozi kama itakavyokuwa ikizungumziwa na Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala Bw. Jumanne Shauri. Hii ni sehemu ya kwanza ya makala hiyo; 

Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala Bwana Jumanne Shauri anaanza kwa kuongelea namna ambavyo kiongozi bora anatakiwa kuwa ili kufanikisha malengo yake anayoyapanga katika kuhudumia  watu anaowaongoza.

Akihojiwa na mwandishi wa jarida hili Mkurugenzi amesema kiongozi lazima awe na dira itakayo muwezesha kupanga mpango mkakati ili kukamilisha dira hizo kwani viongozi waliofanikiwa  hutengeneza dira na kufanikiwa katika uongozi wao kupitia dira walizoziweka.

Dira ni nini?

Dira ni kifaa cha kutambua mwelekeo hivyo dira inapaswa kuonesha muelekeo wa kiongozi wapi alipotoka na ndoto anazotaka kuzifikia. Dira ndio nguzo kuu ya kiongozi itakayo mwezesha kufanikisha malengo yake kupitia mipango ya kimkakati atakayo iweka kwa kulinganisha dira yake na ndoto zake.

Na sio  tu kwa kiongozi bali mtu yoyote ili afanikiwe malengo yake lazima awe na dira na ndoto ili apate muelekeo wa nini anakitaka kukifikia na pia kutengeneza mikakati ya kufikia jambo lake. Katika kuliongelea hilo Bwana Shauri alisema “hata wanafunzi wakitaka kufaulu masomo yake lazima aweke dira kwamba anataka kufikia ufaulu gani mathalani ufaulu wa daraja la kwanza kisha aweke mikakati ni namna gani anaweza kufikia mafanikio hayo”.

Pia Mkurugenzi anasema ” mtu huwezi kukurupuka tu na kusema leo unataka kukimbia mbio za riadha kama hauna maandalizi hivyo ni lazima ujiandae kwa muda hata miezi sita au  ndani ya mwaka mmoja ndipo uweze kushiriki riadha na kufanikiwa kushinda”

 

DIRA ZA VIONGOZI TANZANIA

Tangu awamu ya kwanza ya uongozi wa nchi Tanzania, viongozi wake wote walikua na dira waliozitumia katika kuhudumu muda wote wa uongozi wao na kufanikisha mengi kwa kufuata dira hizo.

Tangu nchi ipate uhuru mpaka sasa Tanzania ina awamu tano za uongozi na awamu zote viongozi wake walihudumu kwa mafanikio makubwa kwa kutumia dira za maendeleo na mipango ya kimkakati ya kufikia dira hizo

Awamu ya kwanza ya uongozi Tanzania chini ya Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ulikua na dira ya kupiga vita umasikini, maradhi na ujinga ili kuhakikisha kila mtanzania anakua na maisha bora.

Dira hiyo ilifanikiwa na kuwafanya wananchi kuondokana na ujinga kwa kufanya elimu kuwa bure ili watanzania wote waweze kusoma hata kama wana hali ya umasikini. Watoto pia walipata nafasi ya kufundishwa na walimu wa UPE  na kupata elimu ya msingi iliyowasaidia kujua kusoma na kuandika.mwalimu Julius Nyerere aliamzisha elimu ya kujitegemea kuanzia shule za msingi mpaka sekondari na vyuoni huku lengo la elimu hiyo likiwa ni kuondoa ujinga pamoja na kuwafanya watanzania wasiwe wageni wa mazingira yao na kuyatumia vyema ili kuweza kujiingizia kipato kwa shughuri mbalimbali za kiuchumi kama kilimo, uvuvi pamoja na useremala.

 

Katika suala la kuondoa umasikini Mwalimu Nyerere alianzisha taasisi ya chakula na lishe. Mapema kabisa wakati Dunia ikiwa bado haijui mchango wa lishe bora kwa watoto na hapa Afrika Tanzania ilikuwa nchi ya kwanza kabisa kuanzisha kituo maalumu cha kutafiti na kuishauri serikali juu ya lishe ya watoto na watu wake kwa ujumla (Tanzania Food and Nutrition Centre). Mpaka leo Tanzania inaheshimika duniani kote kwa kuwa na wataalamu wabobezi katika lishe. Mataifa mengi duniani kote huja hapa nyumbani kujifunza namna kituo chetu cha chakula na lishe kinavyochagiza mipango makini ya afya ya ulaji serikalini na kwa wananchi

Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Profesa Lawrence Mseru amewahi kusema kuwa mwalimu Julius Nyerere ndio muasisi wa bima ya afya ya jamii mwaka 1962.Profesa Mseru ameeleza hayo Oktoba 11, 2019 wakati akizungumza katika kongamano la siku mbili la  kumbukizi ya Mwalimu Nyerere lililoandaliwa na taasisi ya uongozi kwa ushirikiano na  UDSM. Amesema japo Serikali wakati huo hakikuwa kubwa kama sasa, lakini Nyerere alijua mahitaji ya wananchi  na changamoto wanazozipata katika  matibabu yao kwa kutokuwa na utaratibu huo. .

Lakini pia katika kupigana vita na adui umasikini mwalimu julius kambarage Nyerere  alianzisha falsafa ya ujamaa na kujitegemea lengo kuu la falsafa hii lilikuwa ni kulifanya taifa la Tanzania kuwa na uchumi wa kujitegemea na kutokuwa ombaomba kwa mabeberu. Kufuatia dhima hiyo mwalimu nyerere alikuja na mipango mkakati mbalimbali ya kuhakikisha sera ya ujamaa na kujitegemea inaikia malengo kwa kumfaidisha kila mtanzania ambapo alianzisha mipango mbalimbali ikiwemo mashamba ya vijiji, pamoja na kuanziaha viwanda ili kuwezesha upatikanaji wa ajira miongoni mwa watanzania ili kuweza kupata kipato cha kujikimu kimaisha.

 

kwa upande wa Rais Mstaafu wa awamu ya pili Mhe. Ally Hassan Mwinyi alikuja na Dira ya kuikomboa nchi katika hali mbaya ya kiuchumi ya nchi yetu kutokana na athari ya vita ya Kagera wakati huo hiyo kuja na kauli mbiu ya RUKSA. Dira hiyo iliangazia kupigania wanyonge na watu wa hali ya chini kwani alitoa ruksa kwa shughuli zote halali zilizokatazwa kufanywa kufanyika bila kuvunja sheria za nchi. Dira hiyo ilifanikiwa kwa kiasi kikubwa.

Rais wa awamu ya tatu Hayati Benjamin Mkapa yeye aliongoza Tanzania chini ya Sera ya ubinafisishaji akilenga Taifa la Tanzania liweze kuingia katika uchumi wa kati katika maendeleo yake. Akiwa madarakani Rais Mkapa alibinafsisha baadhi ya mashirika yanayomilikiwa na Serikali na akatumia sera ya soko huru. Dira yake ilipata msaada wa Benki ya Dunia na shirika la fedha duniani IMF na kuwezesha baadhi ya madeni ya nje ya Tanzania kufutwa. Aidha Mhe. Mkapa alifanya juhudi za kupambana na ufisadi zilizopelekea kuundwa kwa jukwaa la wazi lililoitwa Tume ya Rais juu ya ufisadi iliyokuwa chini ya Jaji Joseph Sinde Warioba na kuongeza msaada katika mapambano hayo.

Awamu ya nne ya Dkt Jakaya Mrisho Kikwete ilikuja na dira ya maisha bora kwa kila mtanzania kwa kuzingatia anapitia na kuboresha kila sekta ili watanzania wote wanufaike na nchi yao kwa kuwa na maisha bora kwanzia daraja la juu mpaka wananchi wa daraja la chini. Mipango hiyo ilifanikiwa kwa kiasi kikubwa kwani watanzania wengi maisha yao yalibadilika na kuwa bora.  Maboresho yalifanyika kwenye sekta ya ulinzi na usalama, huduma za kijamii na sekta ya utalii  pamoja na uwekezaji sekta nyengine muhumu zenye kuleta maendeleo chachu kwa maisha bora ya watanzania.

 Rais wa awamu ya tano wa Jamuhuri ya Muungano wa tanzania Dkt John Pombe Magufuli kupitia sera ya HAPA KAZI TU ametekeleza dira alizoziweka tangu aanze kuhudumu katika kipindi chake na kuhakikisha dira zilizowekwa na Maraisi wa awamu zilizopita zinafikiwa kikamilifu.

Katika kukamilisha sera na dira yake Rais Magufuli anaamini kwamba viwanda vitakua nguzo katika taifa ili kuleta uchumi ulio bora huku ukitengeneza ajira kwa Watanzania wengi. Rais Magufuli amezidi kujikita katika misingi ya baba wa Taifa katika kujenga vituo vingi vya afya ili kutokomeza adui ambae ni maradhi, kaboresha shule nyingi na kujenga na ameweza kutekeleza sera ya Elimu Bure ili kila mtoto wa kitanzania aweze kusoma.

Sambamba na hayo Shauri aliongelea Viongozi wakubwa Duniani ambao walikua na dira katika uongozi wao zilizosababisha kufikia mafanikio viongozi hao ni pamoja na  Mao Zedong wa China, Mahatma Gandhi wa India  na Martin Luther King wa Marekani.

Mahatma Gandhi alikuwa mwanasheria, mwanafalsafa na mtetezi wa haki za binadamu na kiongozi wa juu wa siasa nchini India.Ghandi alifanya kazi kwenye shamba la miwa nchini Afrika Kusini  lakini aliweka dira kwamba akirudi nchini kwake atahakikisha India inapata uhuru. Aidha aliporejea India aliweka mipango ya kimkakati kwa kutumia mbinu ya uasi wa kiraia usio wa vurugu ulioisaidia india kupata uhuru na kuhamasisha mavuguvugu kadhaa ya haki za kiraia na uhuru Duniani.

Naye Mao Zedong alikua ni kiongozi wa Jamhuri ya watu wa China  kuanzia mwaka 1949 na kiongozi wa chama cha kikomunisti cha China tangu 1935 hadi kifo chake 1976. Katika hatua za mwanzo siasa yake ya kiuchumi ilisababisha njaa na vifo vingi wakati wa utekelezaji lakini maono na ndoto za Mao zilikua ni kuipeleka China katika uchumi ambao sasa tunauona. China imekua nchi ambayo ina uchumi wa juu kutokana na sera iliyowekwa na Mao.

Martin  Luther King alikua na dira na ndoto kuwa ipo siku moja Marekani itaongozwa na mtu mweusi na ndoto hiyo ilitimia kwani mnamo mwaka 2009 hadi mwaka 2017 Nchi ya marekeni iliongozwa na mmarekani mweusi Barack Hussein Obama akiwa kama raisi wa awamu ya 44 kupitia chama cha Democratic.

HITIMISHO

Katika kuhitimisha sehemu hii ya kwanza ya makala Mkurugenzi Jumanne Shauri ametolea  mfano jinsi kiongozi wa Taifa letu Dkt. John Pombe Magufuli ametekeleza Dira kwa vitendo baada ya kuahidi kufika kwenye uchumi wa kati  kabla ya mwaka 2025 na hatimaye kufikia malengo hayo ndani ya mwaka 2020, na kusema kuwa hayo yote yamewezakana ndani ya muda mfupi kutokana na ukweli kuwa kiongozi wetu wa Nchi  alipoingia tu madarkani aliingia na sera yake ya HAPA KAZI tu na kuja na mipango ya kimkakati ya kutimiza sera hiyo kwa kuanzisha na kufufua viwanda ili kutoa fursa ya ajira kwa kila mtanzania.

 

Aidha Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala Jumanne  Shauri amezishauri Manispaa kuwa zinaweza kuweka dira ya kujitegemea na kujiendesha kwa mapato binafsi kwani mpaka sasa kuna baadhi ya Manispaa zinajiendesha zenyewe kwa zaidi ya asilimia ishirini (20%)  hivyo wanaweza kuweka dira ya kujitegemea kwa zaidi ya hapo.

Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi