Ujumbe wa Wageni kutoka Jiji la Chongqing Nchini China waitembelea Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam

Ujumbe wa wageni kutoka Jiji la Chongqing nchini China leo tarehe 15 Novemba, 2023 ukiongozwa na Naibu Meya Bw. Shang Kui pamoja na wajumbe wengine 9 umeitembelea Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam na kufanya kikao na baadhi ya wajumbe kutoka idara ya elimu Sekondari, Idara ya ujenzi pamoja na idara ya biashara. 


Katika mazungumzo hayo, ujumbe kutoka Chongqing umeonesha dhamira ya dhati ya kuimarisha urafiki na Jiji la Dar es Salaam pamoja na kuimarisha huduma za Wananchi hususani eneo la elimu kuanzia ngazi ya awali mpaka chuo kikuu, ujenzi wa miundombinu pamoja na kuimarisha huduma za afya.


Mbali na hayo, ujumbe huo umeeleza kwamba wako tayari kushirikiana na Jiji la Dar es Salaam katika kuboresha huduma za wananchi huku wakisisitiza kuimarisha huduma za Wananchi katika maeneo ya uwekezaji na biashara kwani kwa upande wao wanashughuli wanapofanya jijini Dar es Salaam ambazo huboresha maisha ya Wananchi wa Jiji la Dar es Salaam.


Sambamba na hilo wamemshukuru Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam kwa kuwapokea huku wakiomba ziara hii isiwe mwisho ifanyike katika Majiji yote mawili ambapo wamewataka viongozi wa Jiji la Dar es Salaam Mei 2024, kufanya ziara katika Jiji la Chongqing kwani mwezi huo kuna warsha zinazofanyika Jijini humo kwa Nchi ya China na Nchi nyingine za Kirafiki hivyo ujio huo utapelekea Jiji la Chongqing kutambulisha ujumbe kutoka Jiji la Dar es Salaam.


Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Bi. Tabu Shaibu aliweza kutoa shukrani zake kwa wageni hao huku akiahidi kushirikiana nao katika kuboresha huduma za kijamii kwa wananchi wa Jiji la Dar es Salaam.


Aidha, Urafiki huu utasaidia kubadilishana ujuzi na uzoefu na kuiwezesha Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam katika kutekeleza azma ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kukuza uchumi wa nchi yetu katika maendeleo ya sekta ya biashara na uwekezaji pamoja na kuboresha huduma za Wananchi katika sekta ya Elimu na Afya.



Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi