Matangazo

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
UBORESHAJI WA UKUSANYAJI WA MAPATO YA HALMASHAURI.
Katika mwaka wa fedha wa 2014/15 Manispaa ya Ilala imepanga kukusanya jumla ya Sh. 30,000,000,000.00 kutokana  na vyanzo vyake vya ndani, ambapo kwa kipindi cha Julai hadi Machi 2015 zimekusanywa Sh. 21,830,871,622.90 sawa na asilimia  73%  ya lengo la mwaka. Katika mwaka wa fedha wa 2015/16 tumepanga kukusanya Tshs. 58 bilioni.
Halmashauri ya Manispaa ya Ilala iko katika hatua za kuboresha ukusanyaji wa mapato yatokanayo na vyanzo vyake vya ndani. Hata hivyo kwa sasa nguvu kubwa imeelekezwa katika vyanzo Vikuu vya ndani ambavyo ni vinne; Kodi ya Majengo, Leseni za Biashara, Ushuru wa Mabango na Kodi ya Huduma za Jiji.
KODI YA MAJENGO
Inatozwa kutokana na sheria ya fedha ya Serikali za Mitaa ya mwaka 1983 pamoja na marekebisho yake na sheria ya uthamini ya kodi ya majengo ya mamlaka za miji Urban Authority rating Act no. 2 ya mwaka 1983.Sheria hii inasisitiza kila jengo litozwe kodi kiasi kisichopungua shilingi elfu kumi 10,000/=
Kuna aina mbili za viwango vya tozo ya kodi za majengo. Nazo ni
Kodi ya jengo la makazi asilimia 0.15 na Kodi ya majengo ya biashara asilimia 0.20 ya thamani ya jengo husika. Hivyo majengo yote yanayotumika kwa shughuli za makazi na biashara yanatakiwa kulipiwa Kodi ya majengo. Kodi hii hulipwa mara moja tu kwa mwaka. Kila mwaka Manispaa ya Ilala imekuwa ikiongeza kiwango cha ukusanyaji wa kodi hii kutokana na ongezeko la majengo katika eneo lake. Ili kuweza kutambua kiasi unachotakiwa kulipa kwa ajili ya jengo lako.Inasisitizwa kuwa ni vema kulipia kodi yako mapema ili kuepuka usumbufu.
LESENI ZA BIASHARA
Inatozwa kwa mujibu wa Sheria ya fedha Na.5 ya mwaka 2011. Leseni ambazo zinatozwa na Halmashauri ni zile za Kundi B. Ili kuondoa urasimu wa upatikanaji wa Fomu za maombi wafanyabiashara wanaotaka kukata Leseni wanaweza kuzipata fomu hizo kupitia Tovuti ya Manispaa ya Ilala sehemu ya biashara kwa anuani http://ilala.kpk.fi/@business au kwa kufika Arnatoglou Chumba NA. 1 ambapo atafahamishwa kiasi cha ada anachopaswa kulipa.
Baada ya kulipia ada husika Fomu ya maombi inapaswa kurejeshwa Chumba Na. 5 kwa ajili ya kuandikiwa leseni ya Biashara.
Baadhi ya Wafanyabiashara kwa sababu ambazo wanazijua wao wenyewe wamekuwa wakiwatumia watu wanaojiita Mawakala kwa ajili ya kupata leseni. Kiutaratibu Manispaa haina wakala wa Leseni za Biashara. Imebainika kuwa, hao mawakala wasio waaminifu maarufu kwa jina la Vishoka huwapelekea wateja wao leseni feki za biashara za kughushi ambazo hubainika wakati wa ukaguzi.
Rai inatolewa kwa Wafanyabishara wote ambao waliwatuma Watu kuwakatia Leseni kufika katika Ofisi za Manispaa ya  Ilala ili kufanya uhakiki wa leseni zao endapo ni halali au la.
Kuanzia tarehe 8/04/2015 Manispaa imeanza zoezi la ukusanyaji wa takwimu za majengo na Leseni za Biashara. Zoezi hili litakalofanyika kwa kipindi cha miezi mitatu lengo likiwa ni kupata taarifa na takwimu sahihi za wakazi, wamiliki wa majengo ya biashara na makazi pamoja na wafanyabiashara ndani ya Halmashauri ya Manispaa ya Ilala. Takwimu hizi zitatumika kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi wetu. Aidha linatekelezwa na Maafisa/Watumishi wa Manispaa pamoja na wasaidizi wao ambao ni vijana wapatao 300 walioajiriwa kwa ajili ya zoezi hili. Maafisa hao na Wasaidizi hao wanavyo vitambulisho. Kazi inayofanyika ni kupita katika Mitaa yote kukagua na kuuliza maswali kuhusu taarifa zinazohusu: Jina kamili la mmiliki wa jingo la biashara/makazi, Stakabadhi za malipo ya Kodi ya Majengo yaliyofanyika kwa mara ya mwisho kama zipo na Makadirio ya malipo yaliyofanywa na Manispaa kama yapo. Inaaminika kuwa baada ya kupata takwimu sahihi  Halmashauri itaweza kuboresha takwimu zake na kuweza kukusanya mapato stahiki kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wa Manispaa ya Ilala. Hivyo wafanyabiashara pamoja na Wamiliki wa majengo wanaomba kutoa ushirikiano ili kufanikisha zoezi hili. Utekelezaji wa zoezi hili ni wa kisheria hivyo endapo mtu yeyote atashindwa kutoa ushirikiano au kuwakwamisha Maafisa wanaotekeleza kazi hiyo atachukuliwa hatua za kisheria.
Imetolewa na,
 Ofisi ya Uhusiano
Halmashauri ya Manispaa ya Ilala


1 Maoni

  1. muweke sehemu ya kudownload sheria ndogo ndogo za halimashauli ya manispaa ya ilala

    JibuFuta