Wananchi wahimizwa kula vyakula vya asili

Kuelekea maadhimisho ya Miaka 60 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Halmashauri ya Jiji la DSM kupitia Idara ya Afya imefanya halfa fupi ya kuandaa na kupika Chakula cha asili.


Halfa hiyo imefanyika Leo tarehe 23, Aprili 2024 katika Soko la Kisutu, ambapo mama lishe waliweza kuandaa vyakula vya asili, ikiwa ni mwendelezo wa matukio yanayofanywa na Jiji la DSM kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Sherehe za Miaka 60 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hii ikiwa ni kuhamasisha wananchi lishe bora kwa kuzingatia makundi 6 ya vyakula.


Akiongea kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya, Kaimu Katibu Tawala wa Wilaya Ya Ilala Bi. Flora Mgonja amewataka wazazi na walezi wa kuzingatia utoaji wa lishe bora kwa watoto huku akihimiza utumiaji wa vyakula vya asili.


Amesema “Ajenda hii ya Lishe bora ni ajenda ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hivyo Sisi kama Wilaya ya Ilala tunaendelea kutekeleza agizo hilo kwa kutoa elimu ya lishe kwa wananchi kuzingatia lishe bora na ndio maana leo hii ajenda ya lishe imekua moja ya tukio muhimu katika kuelekea maadhimisho ya Sherehe za miaka 60 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na tumeandaa hafla hii kwaajili ya kuhamasisha ulaji wa mlo kamili huku tukihimiza Watanzania kutosahau asili."


Sambamba na hilo Bi. Mgonja amewapongeza mama lishe wa Soko la Kisutu Kwa kuandaa chakula cha asili kwa kuzingatia taratibu za lishe pamoja na usafi huku akiahidi kulitangaza soko la Kisutu na fursa zinazopatikana kwa wafanyabiashara.

Akiongea katika Hafla hiyo Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Dkt. Zaituni Hamza ameeleza kuwa Idara ya Afya itaendelea kusimamia afua za lishe kama Mhe. Rais anavyosisitiza kwani hakuna maendeleo bila afya bora na afya bora hutokana na ulaji wa lishe bora na mlo kamili.



Kwa upande wake Afisa Lishe wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Bi. Flora Mgimba ameeleza kuwa “Katika kuelekea kilele cha sherehe za miaka 60 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam tumeandaa hafla ya kutayarisha mlo kamili unaoendana na vyakula asili vya Tanzania hivyo katika hafla hii tumewatumia mama lishe na baba lishe ambao tumewajengea uwezo wa namna ya kuandaa chakula katika hali ya usafi na usalama kwa ustawi wa afya zetu huku tukiendelea kutekeleza Afua za Lishe kama Rais Wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoelekeza."


Naye Mwenyekiti Mama Lishe wa Soko la Kisutu Bi. Pendo Mtiti amewashukuru viongozi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kwa kuandaa hafla hiyo huku akiahidi kushirikiana na mama lishe wengine kutoa elimu ya lishe kwa wananchi wengine na namna ya kuandaa mlo kamili katika hali ya usafi kwa ustawi wa afya zetu.

Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi